Ayat al-Ghibah

Kutoka wikishia
Ayat al-Ghibah

Ayat al-Ghibah (Kiarabu: آية الغيبة)(Aya kusengenya) ni Aya ya 12 katika Surat al-Hujurat inabainisha kwamba, kusengenya ni haramu. Katika Aya hii kitendo cha kusengenya kimefananishwa na mtu kula nyama ya nduguye aliyekufa, na kama ambavyo mtu anachukia kula nyama ya ndugu yake aliyekufa, basi vivyo hivyo anapaswa kuchukia kusengenya.

Aya hii ilishuka kuhusiana na watu wawili miongoni mwa masahaba wa Mtume (s.a.w.w) ambao walimsengenya Salman al-Farsi na Usamah bin Zayd.

Kutumiwa neno "ndugu" katika Aya hii ni kutokana na kuwa, kwa mujibu wa Aya ya 10 ya Surat al-Hujurat inayojulikana kama Aya ya Udugu (Ukhwah) ambayo ndani yake inasema kuwa, Hakika waumini ni ndugu. Kwa mtazamo wa baadhi ya wanazuoni wa sheria za Kiislamu (Fikihi) ni kuwa, kwa mujibu wa ibara ya: ((لَحْمَ أَخِیهِ مَیْتاً)) "Nyama ya ndugu yake aliyekufa" iliyokuja katika Aya hii, ni haramu kumsengenya Mwislamu tu na kwamba, inajuzu (mubah) kumsengenya kafiri na hata fasiki; mkabala na mtazamo huo, kuna mafakihi na wanazuoni ambao wanaamini kwamba, kutokana na ukatazwaji jumla "umumiyah" wa kusengenya katika Aya hii, ni haramu pia kuwasengenya wasiokuwa waumini. Ayatullah Makarim Shirazi anasema, kwa mujibu wa Aya hiyo, dhana mbaya ni chimbuko la kufanya ujasusi na kuchunguza mambo ya watu, kuchungunza mambo ya watu hupekea kufichua aibu na siri za watu na kufahamu aibu za watu huwa sababu ya kusengenya; ni kutokana na sababu hiyo, ndio maana dini ya Uislamu imetakaza mambo haya matatu.

Andiko na tarjumi ya Aya

Aya ya 12 ya Surat al-Hujurat inatambulika kwa jina la Ayat al-Ghibah (kusengenya). [1]

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اجْتَنِبُوا كَثِيرًا مِّنَ الظَّنِّ إِنَّ بَعْضَ الظَّنِّ إِثْمٌ وَلا تَجَسَّسُوا وَلا يَغْتَب بَّعْضُكُم بَعْضًا أَيُحِبُّ أَحَدُكُمْ أَن يَأْكُلَ لَحْمَ أَخِيهِ مَيْتًا فَكَرِهْتُمُوهُ وَاتَّقُوا اللَّهَ إِنَّ اللَّهَ تَوَّابٌ رَّحِيمٌ

Enyi mlio amini! Jiepusheni na dhana nyingi, kwani baadhi ya dhana ni dhambi. Wala msipelelezane, wala msisengenyane nyinyi kwa nyinyi. Je! Yupo katika nyinyi anaye penda kuila nyama ya nduguye aliye kufa? Mnalichukia hilo! Na mcheni Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kupokea toba, Mwenye kurehemu.
(Quran: 49: 12)

Sababu ya kushuka kwake

Kumenukuliwa sababu mbili kuhusiana na kushuka Aya ya kusengenya ambayo imeshuka Madina. [2]

  • Tabarsi (aliaga dunia: 548 AH) anasema katika Maj'maa al-Bayan kwamba, Aya hii ilishuka kuhusiana na watu wawili miongoni mwa masahaba wa Mtume (s.a.w.w) ambao walimsengenya Salman al-Farisi. Watu hawa wawili walimtuma Salman kwa Mtume ili akawaletee chakula. Mtume (s.a.w.w) akamtuma Salman al-Farisi kwa Usamah bin Zayd aliyekuwa mtunza stoo. Usamaha akamwambia Salman chakula kimekwisha na Salman akarejea mikono mitupu. Watu wale wawili waliokuwa wamemtuma Salman wakasema Usamah ni bakhili na wakasema kuhusiana na Salman kwamba, kama tutamtuma katika kisima cha Samiha (jina la kisima chenye maji mengi) kitakauka. Kisha wao wenyewe wakaondoka na kuelekea kwa Usamah ili kuchunguza (kufanya ujasusi) kuhusiana na suala hilo. Mtume (s.a.w.w) aliwaambia: Imekuwaje naona athari ya nyama katika midomo yenu? Wakasema: Eeh Mtume wa Allah! Leo sisi hatujala nyama. Mtume akasema: Nyinyi mpo katika hali ya kula nyama ya Salman na Usama! Baada ya hapo ikashuka Aya ya kusengenya (Ayat al-Ghibah). [3]
  • Imenukuliwa kwamba, ((وَلایَغْتَبْ بَعْضُکُمْ بَعْضاً)) yaani wala msisengenyane nyinyi kwa nyinyi, ilishuka kuhusiana na mmoja wa mahadimu wa Mtume (s.a.w.w) ambaye wakati masahaba walipokuwa wakienda kumuona Mtume alikuwa akitaka chakula kutoka kwao na kisha alikuwa akiwazuia kukutana na Mtume. Ni kwa kuzingatia hilo akawa akiitwa bakhili mlaini wa ulimi na Aya ilishuka kumhusu yeye.

Nukta za kitafsiri

Ibn Abbas amesema katika kufasiri Aya hii kwamba, kama ambavyo Mwenyezi Mungu ameharamisha kula nyama ya maiti, ameharamisha pia kusengenya. [5] Kwa mujibu wa Aya hii, kama ambavyo mtu anachukia kula nyama ya mtu aliyekufa, basi vivyo hivyo anapaswa kuchukia kusengenya. [6] La kwanza linapingana na maumbile ya mwanadamu na la pili linakinzana na akili na sheria. [7] Allama Muhammad Hussein Tabatabi anaashiria «فَكَرِ‌هْتُمُوه» yaani "Mnalichukia hilo" na kusema kuwa, kuchukia kula nyama ya ndugu aliyekufa ni jambo lisilo na shaka na hapana shaka kuwa, hakuna mtu anayefanya jambo kama hili. Hivyo basi, kumsengenya ndugu muumini pia linapaswa kuchukiwa; kwani hilo nalo ni mithili ya kula nyama ya ndugu aliyekufa. [8] Imam Khomeini ameserma katika kitabu chake cha Sherh Chehl hadis (Ufafanuzi wa Hadithi 40) kwamba: Kula nyama ya ndugu aliyekufa ni sura ya kibatini ya kusengenya na huko Akhera usengenyaji utajitokeza na kudhihiri katika hali hii. [9]

Imeelezwa kuhusiana na ushabihisjaji na ufananishaji wa kusengenya na kula nyama ya maiti kwamba, kama ambavyo mtu akila nyama ya maiti, maiti hahisi kitu chochote, vivyo hivyo katika kusengenya, kama mtu atamsengenya mwingine na akamsema vibaya, msengenywaji hahisi chochote. [10] Allama Tabatabai anasema kuwa, kutumiwa neno "ndugu" katika Aya kunatokana na kuwa, kabla ya hapo, yaani Aya mbili za kabla yake (Aya ya 10 katika Surat al-Hujurat), waumini wanaelezwa kuwa ni ndugu. Kutumiwa neno maiti nako ni kwa sababu mwenye kusengenywa hana habari kwamba, anasengenywa. [11]

Ayatullah Makarim Shirazi anasema katika Tafsiri Nemooneh kwamba, kwa mujibu wa Aya hiyo, dhana mbaya ni chimbuko la kufanya ujasusi na kuchunguza mambo ya watu, kuchungunza mambo ya watu hupelekea kufichua aibu na siri za watu na kufahamu aibu za watu huwa sababu ya kusengenya; ni kutokana na sababu hiyo ndio maana dini ya Uislamu imetakaza mambo haya matatu. [12]

Matumizi ya Kifikihi

Mafakihi wametaja hukumu za kusengenya kwa mujibu wa Aya ya kusengenya ambazo ni:

  • Mafakihi wanatumia Aya hii kwa ajili ya kuharamisha kusengenya. [13] Kumetolewa fasili na maana tofauti kuhusiana na al-Ghiba (kusengenya) [14]. Allama Tabatabai anasema, upande wa ushirikiano wa yote haya ni kusemwa kitu kumhusu mtu fulani wakati hayupo na pindi akisikia kuhusiana na hilo atakasirika. [15]
  • Kusengenya kutokana na kuwa ni jambo na kitendo kisichofaa katika Aya kimeshabihishwa na kula nyama ya maiti. Kitendo hiki kinahesabiwa kuwa ni katika madhambi makubwa. [16]
  • Imeelezwa kuwa, kuharamishwa kusengenya katika Aya kunahusiana na kuwasengenya Waislamu tu; kwani ibara ya: لَحْمَ أَخِيهِ مَيْتًا (yaani nyama ya nduguye aliye kufa) haijumishi kafiri. [17] Kadhalika ibara ya "nyinyi kwa nyinyi" iliyokuja katika Aya inajuzisha kumsengenye kafiri. [18]
  • Baadhi ya mafakihi wanaona kuwa kwa kuzingatia ukatazwaji jumla "umumiyah" wa kusengenya uliokuja katika Aya hii, ni haramu pia kuwasengenya wasiokuwa waumini; [19] hata hivyo kwa mtazamo wa baadhi ni kuwa, Aya hii inajumuisha tu katazo la kuwasengenya waumini. [20]
  • Kumsengenya fasiki kwa mujibu wa ujumla wa Aya kumeondolewa (hakujajumuishwa) na hivyo kunahesabiwa kuwa inajuzu (mubah) kumsengenya. [21].