Ubebaji mwenge (ada ya kidini)

Kutoka wikishia

Ubebaji mwenge ni mojawapo ya ada na mila za maombolezo ya Muharram nchini Iran na Iraq. Ada hii ya kidini hii hufanyika zaidi katika kumi la kwanza la Muharram huko Iraq na maeneo ya kati na kusini mwa Iran. Katika ada hii ya kidini mioto ya mwenge au mienge huwekwa katika mitaa na viwanja na mahali patakatifu.

Historia yake

Hakuna taarifa sahihi kuhusu umri wa mila hii ya uwashaji na ubebaji mienge. [2] Baadhi ya watu wanasema kuwa historia yake inarejea nyuma hadi takriban miaka mia tano iliyopita. [3] Katika nyakati na duru mbalimbali za historia, ikiwa ni pamoja na wakati wa utawala wa Reza Shah Pahlavi nchini Iran ada hii ya kuwasha mienge katika kipindi cha Muharram ilipigwa marufuku. [4] Katika baadhi ya maeneo, ada hii inajulikana kwa majina mengine. Kwa mfano huko Ardakan katika mji wa Yazd (Iran), ada hii inafahamika kwa jina la taklifu. [5]

Namna inavyofanyika

Ada na mila ya uwashaji, ubebaji na uwekaji mienge katika mitaa na maeneo matakatifu hufanyika kwa njia tofauti katika mikoa tofauti. Katika mtindo wa Kinajafi, mashimo madogo ya mbao au chuma hutumiwa kutengeneza muundo ambao huitwa mash'al (mwenge). Wakati wa maombolezo, mashimo hayo huwashwa moto ndani yake na mienge yake kuwekwa katika barabara za umma za viwanja kuu vya jiji na eneo la nje la mahali patakatifu. Kutokana na uzito mkubwa wa mienge, inahitaji uwezo mkubwa wa kimwili na nguvu za kuibeba. Mienge ni tofauti kwa ukubwa na umbo. [6] Katika baadhi ya maeneo, kama vile Karbala na Ardakan Yazd, wakati mwingine badala ya kuwa na mashimo kadhaa ya moto yenye mipini mirefu, hutumiwa vitu mfano kama vile bendera, badala ya muundo uliotajwa wa mienge mingi. Mwenge huu husogezwa na waombolezaji na katika baadhi ya maeneo, hasa na masharifu pamoja na kukariri mashairi fulani. Kwa kawaida sambamba na kushika mienge hiyo, hupigwa ngoma na matoazi na kuimba mashairi. [7]

Kuenea kijiografia

Ada hii ya kidini inafanyika katika baadhi ya miji ya Iran na Iraq. Huko Iraq, mara nyingi mienge huwashwa na kubebwa katika miji ya Najaf, Kadhmein na Karbala. [8] Nchini Iran pia ada hii hufanyika zaidi katika mikoa ya kati na kusini na miji kama vile Qom, Shahr Rey, na Ardakan katika mkoa wa Yazd, na mara nyingi hufanywa na Waarabu. [9]

Wakati wa kufanyika kwake

Ada ya kubeba mwenge hufanyika katika mikoa tofauti kwa siku tofauti za kumi la kwanza la mwezi Muharram (Mfunguo Nne). [10] shughuli hii mara nyingi hufanywa usiku wa Ashura. Katika mji wa Najaf huko Iraq wakazi wa mji huo hubeba mienge katika usiku wa 8, 9 na 10 Muharram. Katika baadhi ya maeneo, kama vile Ardakan huko Yazd (Iran), ada hii hufanyika katika siku ya kwanza ya Muharram, kwa ajili ya kutangaza mwanzo wa Muharram na kuwaalika watu kushiriki katika majlisi (vikao) vya kuomboleza. [11] Katika baadhi ya maeneo mengine pia, ada ya kubeba na kuweka mienge katika maeneo maalumu hutekelezwa kuanzia usiku wa Tasu'a (siku ya tisa ya Muharram) hadi asubuhi ya Ashura (siku ya kumi) ya mwezi Muharram (Mfunguo Nne). [12]