Mauaji ya Halaiki ya Speicher

Kutoka wikishia

Mauaji ya Speicher ni mauaji ya umati ya Mashia nchini Iraq yaliyotokea Juni 2014 na ambayo yalifanywa na kundi la kigaidi la Daesh (ISIS). Katika tukio hiilo, wapiganaji wa Daesh waliwakamata mateka wanajeshi 1,700 hadi 4,000 wa Iraq na wakawauwa Mashia miongoni mwao.

Waarabu watiifu kwa Chama cha Baath cha Iraq, na manusura wa familia ya Saddam Hussein, rais wa zamani wa Iraq, ni miongoni mwa wanaotuhumiwa kushirikiana na kundi la kigaidi la ISIS katika mauaji haya. Baada ya kuwaua wahanga hao, wanajeshi wa ISIS walizika miili yao kwenye makaburi ya halaiki au kuitupa kwenye mto Tigris, na kulingana na baadhi ya ripoti, walizika kundi la mateka hali ya kuwa wako hai. Daesh walikuwa wakirekodi filamu ya mauaji haya na kuzisambaza. Maafa haya ya kibinadamu yametajwa kuwa moja ya motisha za Wairaqi kuunda Harakati ya Wananchi ya Hashd al-Shaabi. Baada ya tukio hili, serikali ya Iraq iligundua makaburi mengi ya halaiki ya wahanga wa tukio hilo. Baadhi ya watuhumiwa wa tukio hilo pia walikamatwa na kuhukumiwa kunyongwa na kufungwa jela.

Umuhimu na nafasi yake

Mauaji ya umati ya Speicher yametajwa kuwa mauaji makubwa zaidi ya Daesh katika kipindi cha uhai wa kundi hili la kigaidi. Vyanzo vingine vinachukulia tukio hili kuwa tukio kubwa zaidi la kigaidi baada ya mashambulizi ya Septemba 11. [1] Kuna kundi la watu pia ambalo linatafuta kusajili mauaji haya kama mauaji ya kimbari dhidi ya Mashia. [2] Idadi ya watu waliouawa katika maafa haya ni mara kadhaa ya idadi ya watu waliouawa katika operesheni za kigaidi za Daesh barani Ulaya. [3] Idadi kubwa ya takwimu iliyotolewa kuhusiana na maafa haya ni watu 2,500 [4] kati ya mateka 4,000 [5].

Tukio lilivyokuwa

Kwa mujibu wa mmoja wa wanajeshi walionusurika katika mauaji hayo, saa 4:00 usiku mnamo tarehe 12 Juni 2014, licha ya kukaliwa kwa mabavu mikoa miwili Mosul na Salahuddin na kundi la Daesh, takriban watu 3000 walihamishiwa katika kambi ya Speicher, kituo kikubwa zaidi cha anga nchini Iraq. Kwa amri ya kamanda wa kambi hiyo, siku hiyo watu wote walikuwa wamepewa likizo ya siku 15 na kwenda makwao. Baada ya wanajeshi hao kuondoka kwenye kambi hiyo, baada ya muda kidogo walikamatwa na wapiganaji wenye silaha wa Daesh na kupelekwa katika ikulu ya rais mjini Tikrit. Katika ikulu, baada ya uchunguzi wa muda mrefu na kuhojiwa, wanajeshi ambao walikuwa ni Mashia walitenganishwa na wasiokuwa Mashia na kisha Mashia waliuawa. Watu wengine waliosalia walikuwa wakingojea Mahakama ya Sharia ya Kiislamu ya ISIS itangaze uamuzi na hukumu yao. [6]

Mtu mwingine aliyenusurika katika tukio hilo anasimulia kwamba, sababu ya kuondoka kwa wanajeshi hao ilikuwa ni kutoroka na kukimbia kwa wanajeshi 3,000 kutoka katika kambi hiyo ambapo hatimaye walitekwa na wapiganaji 50 wa Daesh. [7]

Kulingana na vyanzo vingine, vikosi vya jeshi vilivyosafirisha askari hadi ikulu ya rais vilitoka kwa makabila yenye silaha ya watu wa eneo hilo, na waliwakabidhi wanajeshi hao katika ikulu ya rais kwa vikosi vya Daesh. [8] Tarehe 12 Juni 2014, kundi la Daesh liliteka na kuchukua udhibiti wa kambi ya kijeshi ya anga ya Speicher. [9] Baada ya hapo, vikosi vya Iraq vilipambana na wapiganaji wa Daesh. [10] Makabila ya Waarabu yalifanya mkutano kuhusu hatima ya wanajeshi waliotekwa katika ikulu ya rais, na kwa kutumia hoja kwamba serikali ya Baath itatawala Iraq hivi karibuni, watawaua kwa umati Mashia ili kupunguza idadi ya Mashia wa Iraqi. Kwa mujibu wa uamuzi huu, tarehe 12 Juni, mauaji dhidi ya Mashia waliokuwa mateka yataanza. Tarehe 13 Juni, Daesh waliingia katika ikulu ya rais na kukabidhiwa mateka. Makamanda wa ISIS walianzisha mahakama ya Sharia na kuwahukumu kifo wanajeshi ambao walikuwa ni Mashia na kuwaachilia huru Masuni waliokuwa wakitubu. [11]

Wakati wa kutekeleza mauaji hayo ya umati dhidi ya wanajeshi Mashia, wapiganaji wa Daesh walikuwa wakirekodi video za mauaji na kuziweka katika mitandao ya kijamii. Wanajeshi walikuwa wakipigwa risasi kichwani na miili yao kutupwa katika Mto Tigris. Katika maeneo mengine, askari walipigwa risasi wakiwa wamefungwa mikono. [12] Kundi la askari walioweza kutoroka kutoka katika umateka wa ISIS, hatimaye walikuwa wakikabiliwa na vurugu za madhehebu ya koo za Waarabu na kuuliwa [13]. Wapiganaji wa kundi la kigaidi la Daesh waliwazika wahanga hao katika makaburi ya umati. [14] Na katika matukio mengine, waliwazika wakiwa hai. [15] Vyombo vya habari vya Iraq viliripoti kwamba, mpaka 21/03/2018, idadi ya miili ya wahanga wa mauaji ya kambi ya Speicher iliyokuwa imepatikana ilikuwa 1150. [16]

Wahanga

Idadi ya wanajeshi waliokamatwa na kundi la Daesh kutoka katika kambi ya Speicher imeripotiwa tofauti. Takwimu zimetaja kutoka kwa wanafunzi wa mafunzo ya kijeshi 1,700 hadi 4,000 wasio na silaha ambao walikuwepo kwenye kambi hiyo wakati ilipotekwa. [17] Lakini tangazo rasmi la magaidi wa Daesh linaripoti kwamba Mashia 1,700 waliuawa katika mauaji haya ya halaiki. Shirika la Kutetea Haki za Binadamu lilitangaza kuwa, idadi ya watu waliouawa katika shambulio hilo ni 2,134 [19].

Matokeo

Miili ya wahanga

Baada ya kukombolewa mji wa Tikrit kutoka mikoni mwa kundi la Daesh mnamo Isfand 1393 Hijria Shamsia (Februari mwaka 2015), makumi ya makaburi ya halaiki ya wahanga wa mauaji ya Speicher yaligunduliwa [20] ambapo Khordad 1393 Hijria Shamsia (Mei 2015) mabaki ya miili 597 ya waliouawa na Speicher iligunduliwa makaburini, [21] na miili 80 ya wahanga wa mauaji hayo ilipatikana kwenye kingo za Mto Tigris. [22] Kaburi kubwa zaidi la watu wengi lililogunduliwa hadi sasa lilikuwa na miili 400 ya wale waliouawa katika mauaji haya. [23]

Watuhumiwa

Kwa mujibu wa baadhi ya ushahidi na taarifa, watu kutoka makabila ya eneo na maafisa wa kijeshi wenye mielekeo ya Kibaath walishirikiana na kundi la Daesh (ISIS) katika mauaji haya. [24] Baadhi ya makabila na vikundi vinavyohusishwa na Al-Qaeda, [25] na mabaki ya familia ya Saddam Hussein wanatuhumiwa kushiriki katika uhalifu na jinai hii. [26] Mnamo 27 Agosti 2014, serikali ya Iraq ilitangaza kuundwa kwa kikosi maalumu cha usalama kilichoitwa " Al-Thar Group for the Martyrs of Speicher) " ili kubaini wahusika wa mauaji hayo. [27] Baada ya takribani miezi mitano mwaka huo huo Hijria Sahamsia kundi la kwanza la watu 30 lilitiwa mbaroni. [28] Miezi michache baadaye, hukumu ya kwanza ya mahakama ilitolewa kwa washtakiwa katika kesi, na 9 Juni 2015 watu 24 kati ya washtakiwa walihukumiwa kifo. [29] Katika miezi na miaka iliyofuata mpaka mwaka 2020 mara kadhaa walitiwa mbaroni watu wakihusishwa na jinai hiyo ambapo kuliendeshwa kesi zao na kutangazwa na vyombo vya habari. [30]

Hatua zilizochukuliwa

Kulingana na Idhaa ya Sauti ya Iraq, Sayyid Moqtada al-Sadr, kiongozi wa Harakati ya al-Sadr, baada ya mauaji ya Speicher, mnamo mwezi Khordad 1393 Hijria Shamsia, aliunda kikosi kilichojulikana kwa jina la "Saraya al-Salam" kwa kuunganisha vikundi vingine kadhaa vya wanamgambo. [31] Kutokana na tukio hili, pamoja na fat’wa ya jihadi dhidi ya kundi la Daesh iliyotolewa na Ayatullah Sayyid Ali Sistani, mmoja wa Marajii Taqlidi wa Kishia ni kwamba, ndio mambo yaliyokuwa motisha na msukumo mkuu wa watu wa Iraq kuunda Harakati ya Wananchi wa ya Hash al-Shaabi dhidi ya kundi la la kigaidi la Daesh. [32] Shirika la Kimataifa la Kutetea Haki za Shia liliitaja siku ya mauaji ya Speicher kuwa "Siku ya Kimataifa ya Haki za Shia". [33]

Katika sanaa na vyombo vya habari

Kumetengenezwa filamu za matukio ya kweli kuhusiana na mauaji na jinai ya Speicher, kama vile kumbukumbu za mwandishi wa vita kuhusu shughuli za mwanamke wa Kiiraqi iliyopewa jina la Umm Qusay, [34] "Daesh kutoka Paris hadi Speicher" [35] na filamu ndefu ya matukio ya kweli ya: "Inja zaman istade” (Here Time Is Stopped), iliyotengenezwa na Fotros Media. [36]