Kimbunga cha al-Aqswa

Kutoka wikishia
Makala hii au sehemu ya makala hii ni tukio la siku. Inawezekana kwa kupita wakati, taarifa zikabadilika kwa haraka. Yumkini habari na taarifa za awali zikawa hazina itibari na habari za hivi punde kabisa kuhusu makala hii huenda zisiakisi tukio lote. Tafadhali chukua hatua ya kuboresha makala hii.
Kimbunga cha al-Aqswa

Kimbunga cha al-Aqswa (Kiarabu: طوفانُ الأقصیٰ) ni operesheni ya kijeshi ya vikosi vya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS dhidi ya Israel katika mpaka baina ya Gaza na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu. Operesheni hii ilianza kutekelezwa tarehe 7 Oktoba 2023 na iliendelea kwa siku kadhaa. Kufuatia mashambulio hayo, awali wanamapambano wa Hamas wakiwa na lengo la kukabiliana na uvamizi wa utawala wa Kizayuni wa Israel walishambulia kwa roketi maeneo ya ardhi zinazokaliwa kwa mabavu na baada ya hapo wakaingia katika ardhi hizo zilizoghusubiwa kupitia njia ya ardhini. Kufuatia shambulio hilo, zaidi ya Waisraeli 1400 waliuawa na wengine 3000 walijeruhiwa. Operesheni hiyo ambayo haijawahi kutokea imetathminiwa kuwa ni kipigo kwa utawala wa Kizayuni wa Israel. Baada ya shambulio hilo, jeshi la Israel lilifanya mashambulio dhidi ya Ukanda wa Gaza na baada ya mashambulio ya mabomu ya siku kadhaa zaidi ya Wapalestina 2600 waliuawa na wengine zaidi ya 9000 kujeruhiwa. Mauaji dhidi ya raia yaliyofanywa na jeshi la Israel na kushambulia kwa mabomu makazi ya raia yalikabiliwa na radiamali mbalimbali ulimwenguni. Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran na Marajii Taqlidi wengine wa Kishia walitangaza kuwaunga mkono wananchi wa Gaza.

Umuhimu na malengo

Vikosi vya HAMAS Oktoba 7, 2023 vilitekeleza operesheni iliyojulikana kwa jina la Kimbunga cha al-Aqswa dhidi ya Israel katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu za Palestina. Vyombo vya habari vya Israel viliitambua operesheni hiyo kwamba; haikuwa na mithili wala mfano katika historia na pia ni kushindwa pakubwa utawala huo. [1] Kadhalika kwa mujibu wa baadhi ya vyombo vya habari vikiwanukuu wanajeshi wa Israel waliokamatwa mateka na HAMAS, shambulio hilo lilipangwa na kuratibiwa kwa kipindi cha mwaka mmoja. [2]

Msukumo na sababu ya HAMAS kutekeleza operesheni hiyo

Sababu na msukumo wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS wa kutekeleza shambulio hilo ulielezwa kuwa ni kukomboa ardhi ya Palestina na kukabiliana na uvamizi na ukiukaji wa haki za binadamu unaofanywa kila uchao na Israel. [3] Vyombo vya habari vinavyoiunga mkono HAMAS navyo vilieza kuwa, sababu ya wanamapambano wa HAMAS ya kutekeleza shambulio hilo ni radiamali dhidi ya jinai endelevu za Israel za kuwaua Wapalestina, kuuvunjia heshima Msikiti wa al-Aqswa, kuwashambulia walinzi wake na kuunga mkono Israel hujuma na uvamizi wa walowezi wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina. [4] Katika taarifa iliyotolewa na Kamandi ya Kijeshi ya HAMAS katika siku ya tatu ya vita iliashiria sababu ya shambulio hilo kuwa ni kukabiliana na uvunjiaji heshima unaofanywa na Wazyuni dhidi ya matukufu ya Waislamu, kuzoea utawaala huo kutenda dhulma na kuvamia ardhi ya Palestina. [5]

Utekelezaji wa operesheni

Gaza-Palestina katika ramani

Tarehe 7 Oktoba 2023 vikosi vya Hamas vilivyoko katika Ukanda wa Gaza vilipanga na kutekeleza operesheni ya kushtukiza katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu za Palestina (Israel). Katika dakika za awali, kulivurumishwa maroketi 5000 dhidi ya ardhi hizo zinazokaliwa kwa mabavu na baada ya hapo, wanamapambano wa Hamas walivuka ukuta unaotenganisha Ukanda wa Gaza na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na kushambulia kwa ardhini vitongoji vya walowezi wa Kizayuni. [6] Amri ya kutekelezwa operesheni hiyo ilitolewa na Muhammad Dhaif, mmoja wa Makanada wa Batalioni za Izzudin Qassam, tawi la kijeshi la Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS. Katika saa za awali za shambulio hilo, kundi la raia na wanajeshi wa Kizayuni walitiwa mbaroni na Hamas na kuhamishwa Gaza wakiwa mateka. Kwa kuanza wimbi la mashambulio, Waziri wa Vita wa Israel alitangaza hali ya dharura. [7] Idadi ya wapiganaji walioshiriki katika shambulio hilo kutoka upande wa HAMAS ilielezwa kuwa ni karibu 1000 na maeneo ya operesheni ya kuingia katika ardhi ardhi zinazokaliwa kwa mabavu yalitajwa kuwa ni 15. [8] Kwa mujibu wa takwimu za Israel, mpaka siku ya 12 tangu kuanza mashambulio ya Hamas dhidi ya ardhi zinazokaliwa kwa mabavu, Waisareli 1400 wameuawa na 3500 kujeruhiwa. [9]

Radiamali

Baadhi ya kutangazwa habari ya operesheni hiyo katika vyombo vya habari, Waislamu katika mataifa mbalimbali kama Iran, [10] Afghanistan, [11] na Iraq [12] walijitokeza na kusherehekea ushindi wa muqawama. Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Hizbullah ya Lebanon zilitangaza kuunga mkono shambulio la Hamas. [14] Ayatullah Ali Khamenei, Kiongozi Mkuu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran aliitaja operesheni hiyo kwamba, ni pigo dhidi ya Israel ambalo haiwezekani kulifidia. [15] Ali Reza A'rafi, Mkuu wa Vyuo Vikuu vya Kidini (Hawza) vya Iran alitathmini shambulio hilo kuwa ni tukio kubwa katika ulimwengu wa Kiislamu. [16] Marekani ilituma manowari yake ya kivita kwa ajili ya kuuunga mkono utawala wa Israel na kuzuia mashambulio. [16]

Shambulio dhidi ya Gaza na kuuawa raia

Uharibifu wa shambulio la Israel huko Gaza baada ya dhoruba ya Al-Aqswa

Baada ya Israel kushtukizwa na shambulio la Hamas, ikiwa na lengo la kulipiza kisasi ilishambulia maeneo ya makazi ya raia na ya kijeshi katika Ukanda wa Gaza. Kukata maji na umeme, kushambulia kwa mabomu makazi ya raia, kuwaua raia wasio na hatia, wanawake na watoto, kuwashambulia kwa mabomu wafanyakazi wa sekta ya tiba, hospitali na kutumia silaha zilizopigwa marufuku ni miongoni mwa hatua zilizochukuliwa na Israel kwa ajili ya kukabiliana na vikosi vya muqawama vya Hamas, hatua ambayo imekosolewa vikali na mataifa mbalimbali. [18] Askari wa Israel waliwatangazia wananchi wa Gaza na kuwapa makataa kwamba, wawe wameondoka katika maeneo ya kazkazini mwa Gaza hadi kufikia siku fulani. Hatua hiyo nayo ilikabiliwa na upinzani mkali wa asasi za jumuiya mbalimbali za haki za binadamu. [19]

Katika mashambulio ya Israel ya kujibu mashambulio dhidi yake katika kipindi cha siku 12 za hujuma na mashambulio dhidi ya Gaza, zaidi ya nyumba 350 za makazi ya watu zimebomolewa na baadhi ya vitongoji vya Gaza vimetokomezwa na kusawazishwa na ardhi. Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya ya Palestina, kufuatia shambulio hilo zaidi ya watu 3,200 waliuawa na wengine zaidi ya 11,000 kujeruhiwa. [20] Shirika la Habari la Marekani NBC lilitangaza tarehe 18 Oktoba 2023 kwamba, idadi ya Wapalestina waliouawa ni 3478 na waliojeruhiwa ni zaidi ya 11,000. [12] Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya ya Palestina hadi kufikia siku ya 11 ya shambulio la Israel, wanawake 500 na takribani watoto 700 walikuwa wameuawa na Israel. [22] Kadhalika kwa mujibu wa ripoti ya Euro News, misikiti 7 ilibomolewa huko Gaza kufuatia mashambulio ya anga ya ndege za kivita za Israel. [23]

Upinzani katika mataifa mbalimbali

Baada ya mashambulio ya utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya gaza, kulianza kufanyika maandamano makubwa katika maeneo mbalimbali ya ulimwengu wa Kiislamu na mataifa yasiyo ya Kiislamu. Uturuki, Iran, Malaysia, Australia, Uingereza, Nigeria, Afrika Kusini na Marekani ni miongoni mwa mataifa ambayo yalishuhudia maandamano ya kuunga mkono muqawama wa Palestina. [24]

Radiamali ya Maulamaa na Marajii Taqlidi wa Kishia

Sayyid Ali Khamenei Kiongozi Mkuu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alilaani shambulio na mauaji ya jeshi la Israel katika hotuba yake aliyoitoa. Aidha Sayyid Ali Sistabni, mmoja wa Marajii Taqlidi mwenye makazi yake Najaf Iraq alitoa taarifa ya kulaani mashambulio na jeshi la Israel dhidi ya Gaza. Noori Hamedani, Makarim Shirazi, Jaafar Sobhani, Javad Amoli na Marajii Taqlidi wengine walionyesha radiamali yao kwa shambulio hilo kwa kutangaza kuwaunga mkono wananchhi wa Wapalestina. [25] Ayatullah Khamenei aliyataja mauaji ya Israel dhidi ya Wapalestina kwamba, ni mauaji ya wazi ya kizazi na akatoa wito wa kushtakiwa utawala wa Kizayuni wa Israel na kusitishhwa mara moja mashambulio ya mabomu dhidi ya Gaza. [26]

Shambulio la Israel dhidi ya Hospitali ya al-Ma'madani

Makala asili: Mauaji ya Hospitali ya al-Ma'madani
Mkutano na waandishi wa habari wa Wizara ya Afya ya Gaza katikati ya miili ya mashahidi wa shambulio la kigaidi la Israel kwenye hospitali ya al-Ma'madani huko Gaza

Oktoba 17 Israel ilishambulia kwa mashambulio ya anga Hospitali ya al-Ma'madani iliyokuwa imejaa majeruhi na wakimbizi wa Kipalestina. Katika shambulio hilo inasemekana kuwa, Israel ilishambulia kwa kutumia bomu la Kimarekani la tani moja, [27 ambapo zaidi ya raia 500 waliuawa. [28] Vyombo vingi vya habari vililitambua shambulio hilo la Israel kuwa mauaji ya kimbari. Kadhalika nchi mbalimbali za Kiislamu na zisizo za Kiislamu zilifanya mikusanyiko. Nchini Jordan ubalozi wa Israel ulichomwa moto. [29] Katika baadhi ya nchi kama Iran na Iraq kulitangazwa siku moja au siku kadhaa za maombolezo ya umma. [30]. Nchini Iran rangi ya kuba la Haram ya Imamu Ridha (a.s) imebadilishwa na kuwekwa rangi nyeusi kuonyesha ishara ya huzuni na simanzi. [31]

Madhara ya kiuchumi, kisiasa na kiusalama

Kuporomoka soko la kiuchumi la Israel

Maandamano ya kupinga Uzayuni mjini London na kuunga mkono operesheni ya Kimbunga cha al-Aqswa, yenye kaulimbiu ya "Uhuru wa Palestina".

Kuporomoka vibaya soko la hisa, kupungua thamani ya sarafu na kudhoofika daraja ya itibari ya Israel katika majukwaa ya kimataifa ni miongoni mwa matokeo na madhara yaliyotathminiwa ya shambulio hilo. Kadhalika miongoni mwa madhara mengine ya muda mrefu ya shambulio hilo yaliyotajwa ni kupungua kwa uwekezaji huko Israel. [32]

Kusimamishwa mchakato kuanzishwa uhusiano kawaida kati ya Saudi Arabia na Israel

Kwa mujibu wa baadhi ya ripoti ni kuwa, baada ya operesheni ya Kimbunga cha al-Aqswa, Saudi Arabia imesitisha na kusimamisha mchakato na mipango ya kuanzisha uhusiano wa kawaida na Israel. [33]

Mapigano ya Israel na Hizbullah kusini mwa Lebanon

Katika siku ya pili baada ya shambulio la Harakati ya Hamas, Harakati ya Hizbullah ya Lebanon ilitoa ujumbe wa kuunga mkono operesheni hiyo na kudai kuwa, imeshambulia maeneo matatu ya jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel. [34] Kadhalika Hizbuullah ya Lebanon katika siku ya tatu ikijibu kuuawa wapiganaji wake kadhaa na Israel ilishambulia kwa makombora na mizinga kambi mbili za jeshi la Israel. [35]

Kuanza kuhajiri Wazayuni kutoka katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu

Kwa mujibu wa Kanali ya Televisheni ya al-Alam, baada ya operesheni ya Kimbunga cha al-Aqswa, raia wa kigeni wanaokaa katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu za Palestina waliondoka na kuhajiri kutoka katika ardhi hizo. [36] Kwa mujibu wa Muhammad Hussein Ghadiri Abyaneh, mweledi wa masuala ya kistratejia ni kuwa, kwa kutekelezwa operesheni ya Kimbunga cha al-Aqswa sio tu kwamba, mwenendo wa wahajiri kuelekea katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu ulisimama, bali mchakato wa kuhajiri na kuhama kutoka katika ardhi hizo ulianza. [37]

Vyanzo