Hablullah

Kutoka wikishia

Hablullah (حَبْلُ الله) maana yake ni Kamba ya Mwenyezi Mungu. Hili ni neno lililotumika katika Qur'an ambapo katika Aya ya I'tisam (kushikamana) Mwenyezi Mungu anawataka Waislamu kushikamana na Kamba ya Mwenyezi Mungu na wala wasifarikiane.[1]

Tafsiri Ayashi (aliaga dunia: 320 H) amenukuu riwaya na hadithi ambazo zinawatambulisha Aal Muhammad (kizazi cha Muhammad) au Imamu Ali (a.s) kuwa ni misdaq na kielelezo cha Hablullah (kamba ya Mwenyezi Mungu.[2] Allama Tabatabai pia anaamini kuwa, makusudio ya Kamba ya Mwenyezi Mungu katika Aya inayosema: ( وَاعْتَصِمُوا بِحَبْلِ اللَّهِ جَمِیعًا) «Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja, wala msifarikiane» , kwamba ni Qur'an na Mtume (s.a.w.w). Kadhalika anasema kuwa, makusudio ya ibara: «Na mwenye kushikamana na Mwenyezi Mungu» katika Aya ya 101 katika Surat al-Imran ni kushikamana na Aya za Mwenyezi Mungu na Mtume (Kitabu na Sunna).[3] Katika Tafsiri ya al-Durr al-Manthur ya Suyuti (aliaga dunia: 911 H) mmoja wa wanazuoni na Maulamaa wa Kisuni kumenukuliwa pia hadithi ambazo zinaeleza kwamba, Qur'an, kizazi cha Mtume, ahadi na kumtii Mwenyezi Mungu ni katika mifano na vielelezo vya Kamba ya Mwenyezi Mungu.[4] Tafsir al-Manar moja ya tafsiri za Kisuni, neno Hablullah (Kamba ya Mwenyezi Mungu) limefasiriwa kwa maana ya kuamrisha mema na kukataza maovu.[5]

Fadhl bin Hassan Tabarsi (aliaga dunia:548 H) anasema kuwa, wafasiri wana maoni na mitazamo tofauti kuhusiana na Hablullah (Kamba ya Mwenyezi Mungu). Baadhi yao wameitambua Hablullah kuwa ni Qur'ani, wengine wanasema ni dini ya Uislamu na baadhi ya hadithi zinawatambua Ahlul-Bayt (a.s) kuwa ni Kamba ya Mwenyezi Mungu. Tabrasi anasema, kujumuisha yote hayo ni bora. Akiwa na lengo kuthibitisha nadharia hii anatumia Hadithi ya Thaqalain (Hadithi ya Vizito Viwili) kama hoja yake ambayo ndani yake Qur'ani na Ahlul-Bayt vimetambulishwa na kutajwa kuwa ni Kamba mbili. Katika nukuu yake, badala ya Thaqalain (Vizito Viwili) ametumia ibara ya Hablain (Kamba Mbili).[6]

Ayatullah Makarem Shirazi anasema, mitazamo hiyo iliyotolewa kuhusiana na Hablullah haitofautiani, kwani makusudio ya Kamba ya Mwenyezi Mungu ni kila kitu ambacho kina uhusiano na Mwenyezi Mungu. Uhusiano huu yumkini ukapatikana kupitia Qur'ani, Mtume (s.a.w.w), Ahlul-Bayt (a.s) na vitu vingine.[7] Aidha anaamini kwamba, Kamba ya Mwenyezi Mungu inaashiria jambo hili kwamba, mwanadamu ili aokoke na giza la ujahili na ujinga anahitajia muongozo au Kamba ambayo kwa kushikamana nayo aweze kutoka katika shimbo la mghafala.[8]

Rejea

  1. Surat al-Imran: Aya ya 103.
  2. 'Ayashi, Tafsir al-'Ayashi, juz. 1, uk. 194.
  3. Tabatabai, al-Mizan, juz. 3, uk. 469.
  4. Suyuti, al-Dur al-Manthur, juz. 2, uk. 284-288.
  5. Rashid Ridha, Tafsir al-Qur'an al-Hakim, juz. 4, uk. 39.
  6. Tabrasi, Majma' al-Bayan, juz. 2, uk. 805.
  7. Makarim Shirazi, Tafsir Nemuneh, juz. 3, uk. 29.
  8. Makarim Shirazi, Tafsir Nemuneh, juz. 3, uk. 32.

Vyanzo

  • 'Ayashi, Muhammad bin Mas'ud. Tafsir al-'Ayashi. Mhakiki: Sayyid Hashim rasuli Mahalati. Tehran: Al-matbuu al-Ilmiah, Chapa ya kwanza, 1380 H.
  • Makarim Shirazi, Nashir. Tafsir Nemuneh. Tehran: Dar al-Kutub al-Islamiah, 1374-1373 HS.
  • Rashid Ridha, Muhammad. Tafsir al-Qur'an al-Hakim (Tafsir al-Manar). Al-Haiah al-'Amah li al-Kitab, 199- M.
  • Suyuti, Abdul Rahman bin Abi Bakar. al-Dur al-Manthur. Dar al-Fikr.
  • Tabatabai, Sayyid Muhammad Hussein. al-Mizan fi Tafsir al-Qur'an. Beirut: Muasase al-A'lami li al-Matbu'at, Chapa ya tatu, 1393 H.
  • Tabrasi, Fadhl bin Hassan. Majma al-Bayan fi Tafsir al-Qur'an. Dar al-Ma'rifah.