Aws bin Thabit al-Khazraji

Kutoka wikishia

Aws bin Thabit al-Khazraji (Kiarabu: أوس بن ثابت الخزرجي) ni sahaba wa Mtume (s.a.w.w) ambaye aliuawa shahidi katika vita vya Uhud. Baadhi ya wafasiri wanasema, Aya ya 7 ya Surat al-Nisaa ambayo inazungumzia moja ya masuala ya urithi, ilishuka kuzungumzia ugawaji wa mirathi yake baada ya kuuawa kwake shahidi.

Utambuzi wa shakhsia

Aws bin Thabit bin Mundhir ni kaka yake Hassan bin Thabit mshairi mashuhuri wa zama za Bwana Mtume (s.a.w.w). Yeye anatokana na familia ya Bani Amr bin Malik kutoka katika kaumu ya Bani Najjar katika kabila la Khazraj. Aws alikuweko katika baia ya aqaba mbili [1] na kwa kuhajiri Mtume (s.a.w.w) na kwenda Madina, akawa katika orodha ya Maansari. [2] Alikuwa mwenyeji wa Othman bin Affan katika nyumba yake mjini Madina. [3]

Kwa mujibu wa kauli mashuhuri, Aws aliuawa shahidi katika vita vya Uhud. [4] Riwaya nyingine inamtambulisha Aws bin Thabit Khazraji kwamba, ni miongoni mwa Mujahidina wa vita vya Badr, Uhud na Khandaq na kwamba, kifo chake kimetambuliwa kwamba, kilitokea katika zama za Ukhalifa wa Othman bin Affan. [5]

Tukio la mirathi

Wafasiri wa Qur'ani Tukufu katika kufasiri Aya ya 7 ya Surat al-Nisaa, wamemzungumzia Aws bin Thabit na kushuka kwa Aya hii baada ya kufa kwake shahidi. Kwa msingi huu, ada ya zama za Ujahilia ilikuwa kwamba, mke na watoto wadogo hawakuwa wakirithi [6] na wanawake na mabinti hawakuwa na fungu katika mirathi. [7] Baada ya kuuawa shahidi Aws, mabinamu zake walichukua na kurithi mali zake zote [8]. Mke wa Aws na mabinti zake watatu wadogo walikwenda kwa Bwana Mtume (s.a.w.w). Mtume aliwataka mabinamu wa Aws wasitumie kwanza mali za Aws mpaka kutakapokuja amri ya Mwenyezi Mungu kupitia Wahyi. [9] Walitii amri ya Mtume. Hatimaye ikashuka Aya ya 7 ya Surat al-Nisaa, [10] ambayo inasema:


لِلرِّجالِ نَصیبٌ مِمَّا تَرَکَ الْوالِدانِ وَ الْأَقْرَبُونَ وَ لِلنِّساءِ نَصیبٌ مِمَّا تَرَکَ الْوالِدانِ وَ الْأَقْرَبُونَ مِمَّا قَلَّ مِنْهُ أَوْ کَثُرَ نَصیباً مَفْرُوضاً

Wanaume wana sehemu katika wanayo yaacha wazazi na jamaa walio karibia. Na wanawake wanayo sehemu katika waliyo yaacha wazazi na jamaa walio karibia. Ikiwa kidogo au kingi. Hizi ni sehemu zilizo faridhiwa.
(Quran: 4:7)