Malezi

Kutoka wikishia

Makala hii inahusiana na wasifu kuhusu mafuhumu na maana ya kifikihi na hivyo haiwezi kuwa kigezo cha amali na matendo ya kidini. Kwa ajili ya amali za kidini, rejea katika vyanzo vingine.

Malezi na usimamizi ni uangalizi wa mtoto ambaye hajafikia hatua ya kubaleghe na ambaye hajafikia kiwango cha kujua zuri na baya. Malezi na uangalizi wa mtoto unajumuisha ulezi, kumuandalia chakula kinachofaa, mavazi n.k Kwa mujibu wa fiq'h ya Kiislamu usimamizi na malezi ya watoto madhali mume na mke wanaishi pamoja, basi jukumu ni lao wote wawili na endapo baba na mama wataachana, kwa mujibu wa fat'wa za akthari ya mafakihi, ulezi na usimamizi wa mtoto wa kike ni wa mama mpaka mtoto afikishe umri wa miaka saba na kwa mtoto wa kiume ni wa mama pia mpaka mtoto huyo afikishe umri wa miaka miwili na baada ya hapo baba ana haki ya kupatiwa ulezi wa mtoto; lakini wanazuoni na mafakihi kama Sayyyid Abul-Qassim Khui anasema kuwa, usimamizi wa mtoto wa kiume mpaka miaka saba ni wa mama. Sheria ya kiraia ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imetungwa kwa msingi na mtazamo huu. Kuaga dunia mzazi mmoja kati ya wawili hao ulezi na usimamizi unahamia kwa mwingine. Kwa maana kwamba, akiaga dunia baba basi ulezi na usimamizi unahamia kwa mama na kinyume chake pia. Endapo baba na mama watafariki dunia, malezi na uangailizi wa mtoto unahamia kwa babu mzaa baba. Mtoto huyu anapofikisha umri wa kubaleghe na kufikia hatua ya ukomavu wa akili (kujua baya na zuri), ulezi na usimamizi huo nao hufikia tamati.

Maana

Maana ya malezi katika istilahi ya kifiq'h ina maana ya usimamizi, kutunza na kulea mtoto na kumuandalia chakula na mavazi yanayofaa. [1] Katika fiq'h maudhui hii hujadiliwa katika sehemu ya ndoa na Luqta (pesa ambayo mwenyewe hajulikani) [2] Masuala kama kipindi cha usimamizi na uangalizi, kutoa haki ya malezi, masharti ya mwenye kulea na usimamizi na malezi kwa mtoto yatima ni miongoni mwa mambo ambayo yanazungumziwa katika fikihi ya Kiislamu.

Muda wa malezi

Kwa mujibu wa fiq'h ya Kiislamu usimamizi na malezi ya mtoto madhali mume na mke wanaishi pamoja, basi jukumu ni lao wote wawili, [3] na endapo baba na mama wataachana, ikiwa mtoto ni wa kike au wa kiume, atalelewa na mama mpaka atakapofikisha umri wa miaka miwili; [4] ama kuhusianan na ulezi na usimamizi wa mtoto baada ya miaka miwili, kuna tofauti za kimitazamo baina ya mafakihi. Sahib al-Jawahir anasema kuwa, mafakihi wenbi [5] akiwemo Muhaqqiq Hilli na Allama Hilli wanaamini kwamba, jukumu la ulezi na usimamizi wa binti utabakia kuwa ni wa mama mpaka mtoto huyo wa kike atakapofikisha umri wa miaka saba na baada ya kutimia umri huo, jukumu hilo atakabidhiwa baba; ama kuhusiana na ulezi na uangalizi wa mtoto wa kiume, jukumu la litabakia kuwa ni wa mama mpaka mtoto huyo afikishe umri wa miaka miwili na baada ya hapo, jukumu hilo atakabidhiwa baba. kwa mujibu wa Fatuwa za akthari ya mafakihi, ulezi na usimamizi wa mtoto wa kike ni wa mama mpaka mtoto afikishe umri wa miaka saba na kwa mtoto wa kiume ni wa mama pia mpaka mtoto huyo afikishe umri wa miaka miwili na baada ya hapo baba ana haki ya kupatiwa haki ya kuwa ya kuwa mtoto huyo. [6] Baadhi ya mafakihi wengine kama Sahib Madarik na Sayyid Abul-Qassim Khui wao wanaamini kwamba, ulezi na usimamizi wa mtoto awe ni wa kike au wa kiume ni jukumu na haki ya mama mpaka mtoto huyo afikishe umri wa miaka saba na baada ya hapo atakabidhiwa baba jukumu hilo. [7] Sheria za kiraia za Jamhuri yay Kiislamu ya Iran zimetungwa kwa mujibu wa mtazamo huu wa kifiq'h. [8] Allama Hilli anasema, Sheikh Mufid amelitambua suala la ulezi na usimamizi wa mtoto wa kike mpaka umri wa miaka miwili kwamba, ni jukumu na haki ya mama. [9] Wakati mtoto anapofikisha umri wa kubaleghe na kukua kiakili, awe ni mtoto wa kiume au wa kike, kipindi cha haki ya usimamizi na uangalizi wa baba na mama kwake kinafikia tamati na mamlaka ya maisha yake yapo mikononi mwake. [10]

Kumuona mtoto

Kwa mujibu wa Fatuwa za Marajii Taqlidi kama Muhammad Taqi Bahjat na Nassir Makarem Shirazi ni kwamba, kila mmoja kati ya baba na mama ambaye kipindi cha usimamizi na uangalizi wa mtoto ni cha kwake, hana haki ya kumzuia mzazi mwenziwe kuja kumuona na kumtembelea mtoto, [11] au hata kumsaidia. [12]

Kuhamisha usimamizi na malezi

Mafakihi wengi akiwemo Shahid Thani, Sahib Riyadh na Sahib al-Jawahir wanalitambua suala la usimamizi na malezi ya mtoto kwamba, ni haki na wanasema kuwa, inawezekana kuhamisha na kukabidhi haki hiyo kwa mtu mwingine. [13] Shahid al-Awwal ameandika katika kitabu chakke cha al-Qawaid Wal-Fawaid: Kama mama atakataa kuchukua jukumu la usimamizi na ulezi (likiwa ni la kwake kwa mujibu wa umri wa mtoto) basi baba atakabidhiwa jukumu hilo; lakini kama wote wawili watakataa hilo, jukumu la usimamizi la ulezi litakuwa wajibu kwa baba. [14]

Masharti ya mwenye haki ya malezi

Kwa mujibu wa fiq'h ya Kiislamu mwenye jukumu la malezi na usimamizi awe mwanaume au mwanamke, anapaswa kuwa ni Mwislamu, na mtu huru (asiwe mtumwa). [15] Kadhalika anapaswa kuwa mwenye akili timamu na awe na sifa na ustahiki wa kulea na kuwa msimamizi wa mtoto. [16] Kwa mujibu wa Fat'wa za mafakihi, mama ana haki ya kupewa ulezi na usimamizi wa mtoto (baada ya kuachana na mumewe) madhali hajaolewa na mwanaume mwingine. [17] Sahib al-Jawahir ameandika kuwa, mafakihi wana ijmaa na kauli moja katika hili. [18] Nukta nyingine katika uga huu ni hii kwamba, mama anaweza kuchukua ujira na malipo kutoka kwa baba kwa kulea na kuwa msimamizi wa mtoto. [19]

Malezi ya yatima

Kadhalika angalia: Yatima

Kuaga dunia mzazi mmoja kati ya wawili hao ulezi na usimamizi unahamia kwa mwingine. [20] Kwa maana kwamba, akiaga dunia baba basi ulezi na usimamizi unahamia kwa mama na kinyume chake pia. Endapo baba na mama watafariki dunia wote wawili, malezi na uangalizi wa mtoto unahamia kwa babu mzaa baba. [21] Kama babu mzaa baba hayupo, kwa mujibu wa baadhi ya mafakihi, haki ya kulea na usiamamizi wa mtoto huyo ni itawafikia wana familia na ndugu wengine kulingana na daraja na mpangilio wao katika urithi; hata hivyo baadhi ya wanazuoni kama Yusuf Bahrani mmoja wa mafakihi wa karne ya 12 Hijria na Sahib al-Jawahir wanasema: Haki ya ulezi na usimamizi wa mtoto huyo ni la familia ya baba. [22]. Bahrani ameandika katika kitabu chake cha al-Hadaiq al-Nadhirah: Ikiwa babu mzaa baba hayupo, mtawala wa kisheria (fakihi) akitumia fedha za mtoto huyo atamuainisha msimamizi na mlezi, na kama mtoto hana mali yoyote, ulezi na usimamizi wake ni jukumu la Waislamu na ni wajibu Kifai. [23].

Malezi na usimamizi wa mtoto wa haramu

Kwa mujibu wa fat'wa za mafakihi ni kwamba, usimamizi wa mtoto ambaye amezaliwa kwa njia ya haramu, ni jukumu la wazazi wake halisi (baba na mama). [24] Hata hivyo mafakihi wanaamini kwamba, mtoto wa haramu hawezi kuwarithi wazazi wake. [25] Sahib al-Jawahir ameandika kuwa, mafakihi wana ijmaa na kauli moja kuhusiana na jambo hili. [26]