Kifayat al-Usul (kitabu)

Kutoka wikishia

Kifayat al-Usul ni kitabu kilichoandikwa na Akhund Khorasani (aliyeaga dunia) 1329 H). Kitabu hiki kilichoandikwa kwa lugha ya Kiarabu kinahusiana na Usul-Fiqh. Akhund Khorasan ni mmoja wa wanafunzi wa Mulla Hadi Sabzevari, Sheikh Ansari na Mirza Shirazi na alikuwa mmoja wa Marajii Taqlidi mahiri na watajika katika zama zake. Jina kamili la mwanazuoni huyu ni Muhammad Kadhim Khorasani. Hata hivyo ameondokea kuwa mashuhuri zaidi kwa jina la Akhund Khorasani.

Tangu kitabu cha Kifayat al-Usul kilipoandikwa wakati huo na hadi leo hii kimekuwa kitabu cha kufundishia katika ngazi za juu za masomo ya Hawza (Chuo Kikuu cha Kidini) na vilevile ni mhimili wa mjadala wa masomo ya "Khariji" ya fikihi (darsa ya daraja la juu kabisa ya fikihi) katika Hawza mbalimbali. Kutokana na umuhimu wake wake, kumeandikwa takribani vitabu na makala 200 za kufafanua na kuelezea kitabu hiki. Maudhui na yaliyoandikwa ndani ya kitabu hiki ni muhimu, na yameandikwa kwa umakini na mpangilio wa hali ya juu. Kutumia maneno na ibara fupi kwa ajili ya kubainisha mafuhumu na maana mbalimbali ni miongoni mwa sifa za kipekee za kifasihi za kitabu hiki chenye thamani kubwa.

Kitabu cha Kifayat al-Usul kimetolewa chapa mara kadhaa katika kipindi cha uhai wa mwandishi wake na hata baada ya kufariki kwake dunia. Kadhalika kuna nakala asili iliyoandikwa kwa hati ya mkono ya mwandishi ambayo inahifadhiwa katika maktaba ya Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran). Mwaka 1409 Hijria kitabu hiki kilisahihishwa na kuchapishwa na Taasisi ya Aal al-Bayt na kisha kusambazwa kikiwa na kurasa 554.

Mwandishi Wake

Makala asili: Muhammad Kadhim Khorasani Muhammad Kadhim Khorasani (1255-1329 H) mashuhur kwa jina la Akhund Khorasani alikuwa Marjaa Taqlidi aliyekuwa akiishi Najaf, Iraq na alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wakiunga mkono Harakati ya Kupigania Katiba nchini Iran (The Constitutional Movement). [11] Mulla Hadi Sabzevari, Sheikh Ansari na Mirza Shirazi ni mongoni mwa walimu wake. [2] Akhund Khorasani amevirithisha vizazi vilivyokuja baada yake vitabu vingi katika taaluma mbalimbali kama za elimu ya Usul al-Fiqh, Fiq'h na falsafa. Hata hivyo, athari yake mashuhuri zaidi ni kitabu cha Kifayat al-Usul. Kutokana na kuandika kitabu hicho, Akhund Khorasan amepewa lakabu ya Sahib al-Kifaya.

Umuhimu

Kitabu cha Kifayat al-Usul ni somo la Usul al-Fiq'h na kimekuwa kikitumika kufundishia katika Hawza mbalimbali (Vyuo Vikuu vya Dini) na kumeandikwa vitabu vingi vinavyofafanua kitabu hiki. [4] Katika makala ya utambuzi wa kitabu wa vitabu vya masomo vya Hawza, kuna takribani vitabu, makala na maandiko 200 yaliyoandikwa yakikitaja kitabu cha Kifayat al-Usul. Ahmad Abidi, mwalimu na mhadhiri wa masomo ya "Khariji" (darsa ya daraja la juu kabisa ya fikihi) katika Chuo Kikuu cha Kidini cha Qom anasema: Mpaka sasa hakuna kitabu kilichoandikwa kwa umakini, mpangilio na mbinu ya ubainishaji kama Kifayat al-Usul. Kwa muktadha huo, kitabu hiki kimekuwa mhimili wa vitabu vya kufundishia vya masomo ya juu kabisa "Khariji" ya Usul al-Fiq'h katika Hawza, na kila kitabu kilichoandikwa baada ya hiki, kiliathirika na mbinu, utaratibu na mpangilio wa maudhui wa kitabu hiki. [6] Inaelezwa kuwa, Akhund Khorasani aliandika kitabu hiki kuanzia mwaka 1321 Hijria na kuendelea. [7] Kwa hakika Kifayat al-Usul ni kitabu mashuhuri zaidi miongoni mwa vitabu vya Akhund Khorasani na kimekuwa na umuhimu kuliko vitabu vingine kutokana na kuwa, kimejumuisha humu mitazamo na misingi ya karibuni kabisa ya usul na maudhui muhimu kabisa za elimu ya usul. [8] Kadhalika lengo la kuandika kitabu hiki lilikuwa ni kupunguza mambo ya ziada katika elimu ya Usul. [9] Pamoja na hayo yote inaelezwa kwamba, kitabu hiki kina mjumuiko kamili wa elimu ya Usul.

Mtindo wa Kielimu na Mbinu ya Uandishi

Agha Bozorg Tehrani anasema: Akhund Khorasani aliingiza masuala ya falsafa katika Usul kabla ya Sheikh Ansari, Muhammad Hussein Hairi (mwandishi wa al-Fusul) na Mirza al-Qummi (mwandishi wa al-Qawanin). [11] Inasemekana kwamba, Akhund Khorasani ametumia kanuni 70 za falsafa ya Kiislamu. [12] Miongoni mwa sifa maalumu za uandishi wa kitabu hiki ni kutumia maneno na ibara fupi na maneno machache. Kifayi Khorasani anasema: Katika kitabu cha Kifayat al-Usul, Akhund Khorasani alinukuu rai na mitazamo ya wanazuoni wa elimu ya usul waliotangulia kwa ibara fupi na kisha akabainisha nukta zao imara na dhaifu na baada ya hapo akataja sababu na kubainisha mtazamo na nadharia yake. [13]

Yaliyomo

Kifayat al-Usul kina mjumuiko kamili wa elimu ya Usul al-Fiq'h ambapo kando yake pia kuna mitazamo mipya kabisa ya ki-usul mpaka katika zama za mwandishi kama ambavyo kuna ukosoaji na uchambuzi kuhusiana na rai na mitazamo hiyo. [14] Kitabu hiki kina utangulizi, milango minane na hitimisho.