Dua ya thelathini na nne ya Sahifa Sajjadiya
Dua ya thelathini na nne ya Sahifa Sajjadiya: ni miongoni mwa dua zilizopokewa kutoka kwa Imamu Sajjad (a.s). Kikawaida yeye alikuwa akiisoma dua hii pale alipokuwa katika dhiki au alipowaona watu fulani wakiwa kwenye matatizo na fedhehesha itokanayo na matendo maovu. Katika dua hii, Imamu Sajjad (a.s) anamsifu Mwenye Ezi Mungu kwa sifa yake ya kuwa ni Msitiri wa Aibu (Sattar al-'Uyub), huku akionesha msisitizo juu ya umuhimu wa kujifunza na kuiga sifa hiyo muhimu ya kuwasitiri wengine, kutoka kwa Mwenye Ezi Mungu ambaye ni mwenye kusitiri dhambi za waja wake, huku akiwahimiza waja wa Mwenye Ezi Mungu kurudi kwa Mola wao (kufanya toba). Ufafanuzi wa na uchambuzi kina wa dua hii ya thelathini na nne, unapatikana katika vitabu vilivyotoa tafsiri na ufafanuzi wa Sahifa Sajjadiya. Miongoni mwanvyo ni pamoja na; kitabu kijulikanacho kwa jina la 'Shuhud wa Shinakht', kilichoandikwa kwa lugha ya Kiajemi na Hassan Mamduhi Kermanshahi, na kitabu kiitwacho 'Riyadh al-Salikin', kilichoandikwa kwa lugha ya Kiarabu na bwana Sayyid Ali Khan Madani. Mafundisho Yaliyomo Ndani ya Dua ya Thalathini na Nne Dua ya thelathini na nne, ambayo ni sehemu ya mkusanyiko wa dua za Sahifa Sajjadiyya, ni dua ilikuwa ikisomwa na Imam Sajjad (a.s.) wakati wa kukabiliana na dhiki au alipokuwa akiitathmini hali ya watu walioangukia kwenye masaibu mbali mbali na wale waliokumbwa na udhalili unaotokana na maasi. [1] Kwa mujibu wa maelezo ya mchambuzi wa dua za Sahifa Sajjadiyya, bwana Mamduhi Kermanshahi, katika uchambuzi wake wa dua hii, anasema kwamba; kila tukio duniani humu, huwa ni funzo kwa muumini. Hata hivyo, mafunzo na mazingatio ya kina zaidi, hupatikana kwa kuchunguza hatima ya wale waliokumbwa na athari za vitendo vyao viovu. [2] Sababu ya hili ni kuwa matukio hayo ni kielelezo cha uhakika na ukweli wa kanuni ya malipo ya kila amali itendekayo duniani humu. Hii huonesha uhusiano wa kimfumo uliopo baina ya mpango wa uumbaji (takwin) na mfumo wa sheria za kimungu (tashri’i), na vilevile (udhalilikaji na ukumbwaji wa balaa hizo), huwasilisha taswira halisi ya Siku ya Hukumu. [2] Mafunzo yanayopatikana katika dua hii yameainishwa katika vifungu vifuatavyo: • Sifa maalum kwa Mwenye Ezi Mungu, ambaye ni msitiri wa dhambi. • Sifa ya Mwenye Ezi Mungu ya kuficha aibu za waja wake, ndiyo msingi wa utulivu katika jamii. • Mwingiliano kati ya ungamo la mwanadamu la uvunjaji wa sheria za kimaadili na jibu la kimungu la kusitiri kosa hilo. • Ombi la marekebisho ya kiroho (toba) na kujitolea katika kufuata mwenendo unaokubalika kimaadili (kwa vitendo na kauli njema). • Ombi la kinga dhidi ya hali ya kutojitambua kiroho (ghafla) na hatari ya utegemezi binafsi usio na mwongozo wa Kiungu. • Kupata funzo la kimaadili kutokana na kitendo cha Mungu cha kusitiri mapungufu ya wengine. • Mchakato wa kutubia na kuachana na vitendo viovu. • Mwelekeo wa kihisia wa kuwa na shauku ya Mwenye Ezi Mungu, na wakati huo huo kutafuta hifadhi dhidi ya hali ya kutojitambua kiroho. • Ombi la kumuomba Mwenye Ezi Mungu amrehemu mbora wa viumbe Wake, Muhammad (s.a.w.w) pamoja na Aali zake watoharifu (a.s). • Wajibu wa kutii na kufuata amri za Mtume Muhammad (s.a.w.w) na Aali zake (a.s). [3] Tafsiri Chambuzi za Dua ya Thalathini na Nne Dua ya Thelathini na Nne, ambayo ni sehemu ya maandiko matukufu ya Sahifa Sajjadiya, ni moja ya zilizopata uchambuzi wa kina katika vitabu mbalimbali vilivyofanya kazi ya kufasiri na kuchambua dua zilizomo kwenye kitabu cha Sahifa Sajjadiyya. Ufafanuzi huu umewasilishwa kupitia lugha mbali mbali, ikiwemo lugha ya Kiajemi pamoja na Kiarabu. Katika medani ya lugha ya Kiajemi, uchambuzi wa dua hii unapatikana katika kazi za wanazuoni kadhaa muhimu, kama vile Mohammad-Hassan Mamduhi Kermanshahi kupitia kitabu chake Shuhud va Shenakht, [4] na Sayyid Ahmad Fahri kupitia kazi yake iitwayo Sharh wa Tarjome Sahife Sajjadiyye. [5] Kwenye upande wa maandiko ya lugha ya Kiarabu, dua hii imedurusiwa na kufafanuliwa katika kazi za kitaaluma zifuatazo: Riyad al-Salikin, kazi ya Sayyid Ali Khan Madani, [6] Fi Dhilali al-Sahifa al-Sajjadiya, kazi ya Muhammad Jawad Mughniyyah, [7] Riadhu al-'Arifin, kazi ya Muhammad ibn Muhammad Darabi, [8] na Afaq al-Ruh, kazi iliyofanywa na Sayyid Muhammad Hussein Fadlallah. [9] Aidha, uchambuzi wa kileksika (lexical analysis) wa istilahi zilizotumika katika dua hii umefanywa kupiti kazi kadhaa za ufafanuzi wa lugha, ikiwemo Ta'liqat 'ala al-Sahifa al-Sajjadiya, kazi ya Faid Kashani, [10] na Sharh al-Sahifa al-Sajjadiyya ya Izzu al-Din al-Jaza'iri. [11]
Matini ya Kiarabu Pamoja na Maelezo ya Kiswahili
وَ کانَ مِنْ دُعَائِهِ علیهالسلام إِذَا ابْتُلِی أَوْ رَأَی مُبْتَلًی بِفَضِیحَةٍ بِذَنْبٍ Na ifuatayo ni moja ya dua zake (Amani iwe juu yake), aliyokuwa akiiomba pale anapopata mtihani, au anapomwona mtu fulani anayeaibishwa kutokana na matendo ya dhambi zake. اللَّهُمَّ لَک الْحَمْدُ عَلَی سِتْرِک بَعْدَ عِلْمِک، وَ مُعَافَاتِک بَعْدَ خُبْرِک، فَکلُّنَا قَدِ اقْتَرَفَ الْعَائِبَةَ فَلَمْ تَشْهَرْهُ، وَ ارْتَکبَ الْفَاحِشَةَ فَلَمْ تَفْضَحْهُ، وَ تَسَتَّرَ بِالْمَسَاوِئِ فَلَمْ تَدْلُلْ عَلَیهِ. Ewe Mwenyezi Mungu, shukrani zote ni Zako (nakushukuru) kutokana na ya stara yako (ya kutusitiri uovu wangu) licha ya ujuzi Wako (juu ya uovu wangu), na (nakushukuru) kwa kutusamehe (makosa yetu) licha ya ufahamu Wako wa kina (juu ya makosa hayo). Kwa hakika, kila mmoja wetu amefanya kosa la aibu, nawe katu hukuliweka hadharani kosa hilo (hukumfedhehesha), na (bila shaka kila mmoja wetu) ametenda jambo chafu, lakini Hukumwaibisha (kwa kosa lake hilo), na (badala yake) ukamstiri na ovu hilo, na wala hukumfedhehesha mbele ya wengine. کمْ نَهْی لَک قَدْ أَتَینَاهُ، وَ أَمْرٍ قَدْ وَقَفْتَنَا عَلَیهِ فَتَعَدَّینَاهُ، وَ سَیئَةٍ اکتَسَبْنَاهَا، وَ خَطِیئَةٍ ارْتَکبْنَاهَا، کنْتَ الْمُطَّلِعَ عَلَیهَا دُونَ النَّاظِرِینَ، وَ الْقَادِرَ عَلَی إِعْلَانِهَا فَوْقَ الْقَادِرِینَ، کانَتْ عَافِیتُک لَنَا حِجَاباً دُونَ أَبْصَارِهِمْ، وَ رَدْماً دُونَ أَسْمَاعِهِمْ Ni makatazo Yako mangapi uliyotukataza nasi tukaachana nayo, na ni amri ngapi ulizotuamrisha nasi tukazikiuka na kuivuka mipaka yake! Ni maovu mangapi tuliyoyatenda, na ni makosa mangapi tuliyoyafanya! Hakuna aliyekuwa na khabari kuhusiana na nayo, isipokuwa ni Wewe peke Yako ndiye uliyekuwa na khabari juu ya makosa hayo. Nawe peke Yako Ndiwe mwenye uwezo wa kuyadhihirisha, pasi na wengine wote wenye mamlaka ya kufanya hivyo. Hata hivyo, msamaha Wako kwetu ulikuwa kama pazia mbele ya macho ya walimwengu (yao) na kizuizi mbele ya masikio yao.
فَاجْعَلْ مَا سَتَرْتَ مِنَ الْعَوْرَةِ، وَ أَخْفَیتَ مِنَ الدَّخِیلَةِ، وَاعِظاً لَنَا، وَ زَاجِراً عَنْ سُوءِ الْخُلُقِ، وَ اقْتِرَافِ الْخَطِیئَةِ، وَ سَعْیاً إِلَی التَّوْبَةِ الْمَاحِیةِ، وَ الطَّرِیقِ الْمَحْمُودَةِ Hivyo basi, jaalia kitendo Chako cha kutusitiria aibu zetu na kutufichia maovu yetu ya siri, kiwe ni mawaidha (somo) kwetu. Na (kifanye) kiwe ni kinga inayotuepusha na akhlaqi (tabia) mbovu na kutumbukia makosani. Na kiwe ni msukumo wa kuielekea toba ya kweli (Tawbatan Nasuha), yenye kufuta madhambi, na (iwe ndiyo sababu ya) kuifuata Njia Yako iliyonyooka na yenye kuridhiwa. وَ قَرِّبِ الْوَقْتَ فِیهِ، وَ لَا تَسُمْنَا الْغَفْلَةَ عَنْک، إِنَّا إِلَیک رَاغِبُونَ، وَ مِنَ الذُّنُوبِ تَائِبُونَ.
Na ukurubishe wakati wake (wakati kuyatekeleza hayo), na usitutie katika hali ya kukusahau, hakika sisi ni wenye kukutamani Wewe (ni wenye hamu Nawe), nasi ni wenye kutubu kutokana na madhambi (zetu).